KARIBUNI MCHICHANI

Kwa Habari moto moto Kuhusu Siasa , Uchumi, Maisha, Elimu Na Mengine Mengi.



Friday, September 17, 2010

NAKAAYA AIKACHA CHADEMA,AJIUNGA NA CCM!

Rafiki yangu mmoja aliwahi kuniambia jambo ambalo nilimbishia karibu mishipa ya fahamu initoke.Aliniambia kwamba vuguvugu lililopo nchini la vijana na hususani wasanii wa muziki wa kizazi kipya kujiunga na vyama vya siasa, linaongozwa na utashi wa kishabiki shabiki tu na pia tamaa ya fedha na kujiongezea tu umaarufu fulani katika jamii

Nilimbishia nikiwa na sababu kama vile,kwanza ni haki yao kikatiba na pia wao kama “kioo cha jamii” bila shaka wamekaa chini na kutafakari kwa kina chama au vyama ambavyo wao wanaona vimedhamiria kumkomboa mwananchi wa kawaida kutoka katika matatizo ya kimsingi yanayomkabili.Isitoshe wengi wao ni vijana na kama unavyojua msemo mpya ni kwamba vijana ndio taifa la leo na sio kesho. Pia nilimwambia kwamba ingekuwa suala ni pesa tu,basi wote wangejiunga na CCM kwani let’s face it,jamaa wana hela.Usiniulize wanaipata wapi kwa sababu hata mimi vyanzo vya pesa hizo sivijui kwa ndani.



Leo hii,jioni hii,mwanamuziki Nakaaya Sumari,ambaye miezi kadhaa iliyopita alijiunga na Chama Cha Demokrasia na Maendeleo(CHADEMA) na kukabidhiwa kadi ya uanachama nambari 0227706, amekikacha chama hicho na kujiunga na Chama Cha Mapinduzi(CCM). Kwa mujibu wa Global Publishers, tendo hilo limefanyika jioni mbele ya mgombea uraisi kwa tiketi ya CCM, Jakaya Mrisho Kikwete huko katika Uwanja wa Sheikh Amri Abeid jijini Arusha.

Ni haki yake kufanya hivyo.Hiyo ndio raha na karaha ya demokrasia.Pamoja na hayo,najiuliza,hivi hawa wasanii wanaelewa kweli nguvu waliyonayo katika kujenga au kushawishi fikra za wananchi?Kwa mfano najiuliza,nini kilimsukuma Nakaaya kujiunga na CHADEMA miezi michache tu iliyopita na leo hii kuamua kujiunga na CCM? Je sababu alizozitoa katika uamuzi wake wa kujiunga na CHADEMA miezi michache tu iliyopita zimekwenda wapi?

Nini kinawasukuma vijana wasanii katika siasa?Ni kweli wanakerwa na matatizo yanayowakabili wananchi au nchi kwa ujumla au kuna lingine kama yale aliyonitajia rafiki yangu hapo juu?

Msikilize Nakaaya katika kibao chake kilichompa umaarufu cha Mr.Politician hapo chini.Pengine kuna haja ya kuwa na version ya Ms.Politician pia.

No comments:

Post a Comment